Na mwandishi wetu
Mabondia Seleman Kidunda na Mfaume Mfaume Ijumaa hii watapanda ulingoni kuzichapa na wapinzani wao katika mapambano yanayosubiriwa kwa hamu yatakayofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.
Kidunda atakayepigana pambano la mwisho na Eric Mukadi raia wa DR Congo, amewataka mashabiki wa mchezo huo kujitokeza kwa wingi na kupata burudani halisi ya mchezo huo.
“Nimekuwa na maandalizi mazuri wakati wote wa kujiandaa dhidi ya mpinzani wangu sababu najua halitokuwa pambano jepesi na nilishasema atakavyokuja ndivyo tutakavyompokea maana nipo tayari,” alisema.
“Ubora wangu unafahamika ninapokuwa ulingoni, ninachotaka kuwaambia mashabiki wangu waje kwa wingi Mlimani City, nataka waje waangalie burudani ya ngumi na siyo maneno kama anavyosema mpinzani wangu,” alisema Kidunda.
Naye, Mfaume atakayepigana na Nkululeko Mhlongo wa Afrika Kusini alisema anafahamu kuwa mpinzani wake ana rekodi nzuri lakini ataingia ulingoni kuipambania Tanzania kiujumla kutafuta ushindi.
Promota wa pambano hilo kutoka PAF Promotion Company Ltd, Fadhili Maogola alisema kutakuwa na mapambano mengine manane ya awali kabla ya pambano la Mfaume na la mwisho la Kidunda.
Maogola pia alisema kwamba wakati wa pambano hilo kutakuwa na burudani nyingi za kutosha hivyo Watanzania wajitokeze kwa wingi wafurahi.”
