Na mwandishi wetu
Mshambuliaji kinara wa Simba, Moses Phiri amesema anaendelea vizuri kupona majeraha aliyonayo huku akiahidi punde atakaporejea ataendelea kukipigania kiatu cha ufungaji bora msimu huu.
Phiri aliyeumia Desemba, mwaka jana walipokuwa wakiumana na Kagera Sugar tayari amemaliza zaidi ya wiki moja ya kuuguza majeraha yake na ameshaanza mazoezi ya kurejea kikosini tangu kikosi hicho kilipokuwa kambini Dubai hivi karibuni.
Mchezaji huyo raia wa Zambia, mpaka sasa amefunga mabao 10 akizidiwa mabao matano na kinara Fiston Mayele wa Yanga, ingawa Phiri anaamini atakaporejea atakimbizana naye na kumpiku.
“Mipango yangu ni kwamba nikishapona kabisa ni kupigania nafasi yangu ya kutwaa kiatu cha ufungaji bora na pia kuhakikisha naisaidia vilivyo timu yangu kuhakikisha tunatwaa ubingwa wa ligi,” alisema Phiri.
Pia alisema anafurahi kuongezeka kwa wachezaji wapya waliosajiliwa hivi karibuni akiamini hiyo inaleta afya kwa timu na kuongeza silaha zitakazosaidia timu kupata matokeo wakati wote hata kama wengine watakuwa nje kwa sababu tofautitofauti.
Katika usajili wa dirisha dogo lililofungwa juzi Januari 16, mwaka huu, Wekundu hao wamefanikiwa kunasa saini za washambuliaji Saido Ntibazonkiza kutoka Geita Gold, Jean Beleke (TP Mazembe), Mohamed Mussa (Malindi) na kiungo mkabaji Ismael Sawadogo (Difaa El Jadida).