Na mwandishi wetu
Mshambuliaji Idris Mbombo (pichani) raia wa DR Congo amejiunga na Nkana Red Devils ya Zambia kwa mkataba wa miaka miwili akitokea Azam FC.
Mbombo mwenye miaka 28 amejiunga na Nkana na kukabidhiwa jezi namba 20 baada ya kudumu kwenye kikosi cha Azam kwa misimu mitatu akitokea El Gouna inayoshiriki Ligi Kuu ya Misri.
Hii inakuwa mara ya tatu kwa Mbombo kurejea katika kikosi cha Nkana ambapo amewahi kucheza katika misimu ya 2017/18 na 2019/20.
Akizungumza leo Jumamosi na waandishi wa habari baada ya kutambulishwa, Mbombo alisema amerudi nyumbani, hivyo mashabiki wa Nkana watarajie mazuri kutoka kwake kwani ametua hapo kufanya kazi.
“Hapa ni kama nyumbani nimekuwa hapa kwa nyakati tofauti, mazingira ni rafiki kwangu naushukuru uongozi kwa kuniamini na kunipa nafasi ya kuja kucheza hapa,” alisema Mbombo.
Mbombo amekuwa mchezaji wa kwanza kuachwa na Azam katika dirisha hili la usajili ambalo tayari nafasi yake imechukuliwa na mshambuliaji raia wa Colombia, Franklin Navarro.