Na mwandishi wetu
Kocha Mkuu wa KMC, Thiery Hitimana amesema matumaini ya timu hiyo kushiriki Ligi Kuu NBC msimu ujao ni madogo kutokana na kipigo walichokipata juzi kutoka kwa Geita Gold FC.
KMC inashika nafasi ya 14 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 26, ikiwa imebakiwa na michezo minne kabla msimu kumalizika.
Hitimana ameeleza kuwa wanachokifanya hivi sasa ni kuhakikisha wanashinda michezo hiyo minne iliyobaki ili angalau kuangukia kwenye mechi za mtoano za kuwania kutoshuka daraja sababu uwezo wa kumaliza nafasi za katikati kwa sasa haupo.
“Malengo yetu ilikuwa ni kushinda mechi na Geita na nyingine zilizobaki lakini imekuwa tofauti, mikakati yetu kwa sasa ni kushinda mechi nne zilizobaki pengine zinaweza kutunusuru tusishuke daraja,” alisema Hitimana.
Kocha huyo pia amesema pamoja na kuwa na matumaini madogo lakini wataendelea kupambana ili kuwajengea wachezaji wake uwezo wa kupambana na kufanikiwa lengo hilo.
Hitimana amewaomba wadau wa soka wilaya ya Kinondoni na kuwataka waendelee kuipigania timu yao ili waweze kukaa sehemu salama kwenye msimamo wa ligi hiyo ambayo inashirikisha timu 16.