Manchester, England
Kocha wa zamani wa Man United, Sir Alex Ferguson amelazimika kukimbizwa hospitali Jumapili, Mei 3, 2026 muda mfupi kabla ya mechi ya timu hiyo na Liverpool kwenye dimba la Old Trafford.
Habari zinadai kuwa uamuzi wa kumpeleka kocha huyo hospitali ulikuwa ni sehemu ya tahadhari tu kwa Ferguson mwenye umri wa miaka 84 na si kwamba alikuwa katika hali mbaya sana.
Ferguson alikuwa uwanjani eneo la watu mashuhuri kuishuhudia Man United ikiikabili Liverpool katika Ligi Kuu England na muda mfupi kabla ya mechi kuanza alipigwa picha akiwa na wageni wengine.
Baadaye alichukuliwa katika gari la wagonjwa ambalo lilitoka katika uwanja wa Old Trafford na kumpeleka kocha huyo hospitali ingawa haikuweza kuelezwa undani ya hali aliyopitia kocha huyo hadi kupelekwa hospitali.
Enzi zake akiwa Man United, Ferguson aliinoa kwa mafanikio timu hiyo kwa miaka 27 na alifanikiwa kubeba mataji karibu yote makubwa.
Mwaka 2018, Ferguson alipata matatizo ya ubongo na kuwa katika hali mbaya kabla ya kupata nafuu na miaka mitatu baadaye alizungumzia hali aliyopitia na hatimaye kuwa sawa.
Akizungumza baada ya mechi kocha wa Man United, Michael Carrick ambaye timu yake iliilaza Liverpool mabao 3-2 na kufuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya, alisema anamtakia heri Ferguson apone haraka.
Kimataifa Ferguson akimbizwa hospitali
Ferguson akimbizwa hospitali
Read also
