Na mwandishi wetu
Mkurugenzi wa Ufundi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Oscar Mirambo amesema kwa maandalizi waliyofanya anaamini timu ya taifa ya wasichana chini ya miaka 17, Serengeti Girls, iko tayari kwa ajili ya mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Zambia.
Serengeti wanatarajia kushuka uwanjani Februari 3, mwaka huu dhidi ya Zambia katika mchezo wa kwanza wa kutafuta nafasi ya kufuzu michuano ya Kombe la Dunia chini ya miaka 17.
Mchezo wa marudiano unatarajiwa kupigwa Februari 9, mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es salaam.
“Tumefanya maandalizi mazuri, tumewaandaa vijana kimwili na kisaikolojia, tunaenda kupambana ugenini, tunatarajia kufanya vizuri katika mchezo wetu huo wa kwanza na baadaye tutarudi nyumbani,” alisema Mirambo.
Kikosi cha Serengeti Girls kinachoenda nchini Zambia kinaundwa na makipa Marian Shaban, Mwanaidi Maulid wote kutoka Bunda Queens na Salome Saint (Geita Gold Queens).
Mabeki ni Sarah Joel, Manka Richard (Fountain Gate Princess), Neema Damas (Baobab Queens), Edna Makamba (Oysterbay Queens), Ladia Maximilian (JKT Queens), Masika Mwakisua (Yanga Princess), Sarah Lucas na Kurwa Rockets (Bunda Queens).
Viungo ni Winfred John (Yanga Princess), Ester Maseke, Melikia William, Semeni Juma (Bunda Queens), Naomi Charles, Sabina Alex, Asha Ramadhani (Geita Gold Queens) na Marry Siyame (La Liga Academy, Hispania).
Washambuliaji ni Jamil Rajabu, Yasinta Mitoga, Winifrida Gerald (JKT Queens), Mwantima Mwarabu (Geita Gold Queens) na Jamil Celestine (Bunda Queens).