Yaounde, Cameroon
Shirikisho la Soka Cameroon limeshtushwa baada ya kubaini kuwa serikali kupitia Wizara ya Michezo imemuajiri Marc Brys (pichani) kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya taifa ya soka maarufu ‘Indomitable Lions’.
Brys, kocha kutoka Ubelgiji anachukua nafasi ya Rigobert Song ambaye mkataba wake ulifikia ukomo baada ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon) mapema mwaka huu na hakupewa mkataba mpya.
“Shirikisho la Soka Cameroon sawa na wananchi wengine wote wa Cameroon nalo limesikia kuhusu habari ya uteuzi wa nafasi yenye majukumu kwenye timu ya taifa ya wanaume,” ilieleza taarifa ya shirikisho hilo.
Taarifa ya shirikisho pia ilidai kuwa uamuzi uliofikiwa ni wa upande mmoja na limeeleza kushtushwa kwake na jambo hilo kwani ni kinyume na kanuni na taratibu za shirikisho hilo kuhusu uendeshaji na usimamizi wa timu za taifa.
Taarifa hiyo pia ilifafanua kuwa shirikisho hilo limeamua kuweka wazi jambo hilo la kusikitisha hapo hapo ikieleweka kwamba taratibu za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) haziruhusu serikali kuingilia kwa namna yoyote masuala ya soka.
Song, beki wa zamani wa timu ya taifa ya Cameroon alikuwa kocha wa timu hiyo kwenye fainali za Afcon mapema mwaka huu nchini Ivory Coast ingawa timu hiyo iliishia hatua ya 16 bora.
Kimataifa Mrithi wa Rigobert Song aajiriwa kimya kimya
Mrithi wa Rigobert Song aajiriwa kimya kimya
Related posts
Read also
