Na mwandishi wetu
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imeufungia Uwanja wa CCM Kambarage, Shinyanga unaotumiwa na timu ya JKT Tanzania kama uwanja wa nyumbani.
Kupitia barua iliyotumwa jana Jumatano kwa uongozi wa JKT kutoka TPLB, imeeleza kuwa uwanja huo umefungiwa kuanzia jana Oktoba 3, mwaka huu kwa kukosa vigezo vya kikanuni na sheria za mpira wa miguu.
“Uwanja huo umekosa nyasi za kutosha katika eneo la kuchezea (pitch) pamoja na kutokuwa tambarare jambo linalosababisha mtirirko wa mpira kutokuwa sawa pamoja na kuwa na muonekano usiovutia kwa watazamaji wanaohudhuria uwanjani na wanaotazama michezo ya ligi kupitia runinga,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Barua hiyo iliyosainiwa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi, Almasi Kasongo (pichani juu) imeutaka uongozi huo kuchagua na kutuma jina la uwanja mwingine utakaotumika kwa michezo yao ya nyumbani mpaka yatakapofanywa marekebisho Kambarage kisha kukaguliwa na kuthibitishwa kama unafaa kutumika tena.
Hayo yameibuka baada ya mchezo wa hivi karibuni ambao JKT iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mashujaa, kabla ya hapo uwanja huo ulitumika kwenye mchezo wa JKT na Kagera Sugar ulioisha kwa sare ya bao 1-1.
Soka Uwanja wa CCM Kambarage wafungiwa
Uwanja wa CCM Kambarage wafungiwa
Related posts
Read also