Na mwandishi wetu
Kiungo wa Yanga, Mudathir Yahya amepenya kwenye kinyang’anyiro cha kuwania mfungaji wa bao bora la michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika hatua ya makundi msimu huu.
Wapinzani wa Mudathir katika kipengele hicho ni Aymen Mahous wa USM Alger alipoifunga FC Lupopo, Aubin Kramo wa Asec Mimosas alipoinyoosha Diables Noirs na Paul Acquah wa Rivers United dhidi ya DC Motema Pembe.
Mudathir ameingia kupitia bao lake alilowafunga TP Mazembe kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam katika ushindi wa mabao 3-1 walioupata Yanga katika mechi hiyo.
Mchezaji huyo na Farid Mussa ambao wote wamewahi kukipiga Azam ndio wachezaji pekee wazawa wa Yanga waliofunga mabao katika hatua hiyo ambapo jumla Yanga imefunga mabao tisa na kufungwa manne.
Mabao mengine saba ya Yanga yamefungwa na Fiston Mayele, Tuisila Kisinda, Kennedy Musonda na Jesus Moloko ambao wote ni wachezaji wa kigeni.
Kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika walioingia kwenye kinyang’anyiro hicho ni Hamdou El Houni wa Esperance alipoifunga CR Belouizdad, Mahmoud Karhaba wa Al Ahly walipopepetana na Al Hilal, Makabi Lilepo wa Al Hilal alipoichapa Coton Sport na Teboho Mokoena wa Mamelodi Sundowns walipocheza na Al Ahly.
Upigwaji wa kura unaendelea mpaka kesho Jumatano alasiri kwenye akaunti maalum ya Twitter ya Shirikisho la Soka Afrika (Caf) ya michuano ya Ligi ya Mabingwa na Kombe la Shirikisho Afrika.
Kimataifa Bao lambeba Mudathir Afrika
Bao lambeba Mudathir Afrika
Read also
