Na Hassan Kingu
Ubora wa viwanja vya soka ni eneo muhimu ambalo halipaswi kupuuzwa kwa namna yoyote ile hasa ubora huo unapohusisha eneo la kuchezea yaani pitch.
Mashabiki na wapenzi wa soka wanaweza kujadili matatizo yaliyo mengi kuhusu viwanja hasa vile vinavyotumiwa kwa mechi za Ligi Kuu NBC na wakayapuuza baadhi lakini watakuwa wa ajabu wakipuuza hoja ya ubora wa eneo la kuchezea.
Uwanja unaweza kuwa na vyoo vichache au vyoo ambavyo havipo katika ubora, uwanja unaweza kuwa na tatizo la majukwaa, viti kuharibika na kusababisha mashabiki kusimama, huduma ya maji ikawa ya mashaka, yote hayo yakavumiliwa kwa staili ya funika kombe mwanaharamu apite lakini si tatizo la eneo la kuchezea.
Tatizo la eneo la kuchezea madhara yake ni makubwa na yanatosha kuchangia kupoteza maana nzima ya ushindani kwenye soka, timu inaweza kupoteza mechi kimaajabu au kushindwa kupata ushindi.
Uwanja wenye eneo bovu la kuchezea unapoteza maana halisi ya kuwa uwanja wa soka, mamlaka zisikae kimya kwa uwanja wenye mashimo na miinuko ya ajabu ajabu, usio na majani yaani vipara, hatua lazima zichukuliwe.
Kwa siku za hivi karibuni tumeshuhudia mamlaka za mpira zikivifungia baadhi ya viwanja na kuvifungulia baada ya muda mfupi hatua ambayo inakuwa kero kwa mashabiki wa soka na inawakatisha tamaa hasa pale fungia fungia hiyo inapojirudia mara mbili au hata tatu katika msimu mmoja.
Jaribu kumfikiria shabiki ambaye amejipanga kwenda uwanjani kuangalia mechi baina ya timu yake halafu ghafla uwanja unafungiwa kwa sababu haukidhi vigezo ambavyo havibainishwi kwa mapana kwenye taarifa za mamlaka husika.
Kwa shabiki uamuzi huo ni kero na kero inakuwa kubwa zaidi mechi hiyo inapohamishiwa uwanja mwinghine ambao upo mbali tena wakati mwingine katika mkoa ambao kero si tu kwa shabiki bali kwa uongozi na wachezaji.
Uongozi unajikuta katika gharama nyingine mpya zilizoongezeka za kusafirisha timu wakati kwa wachezaji wanaingizwa katika uchovu wa safari ambao hawakuutarajia na hivyo kuathiri viwanja au ubora wao mchezoni.
Tumesikia fungia fungia hii ya viwanja ikijitokeza katika baadhi ya viwanja vikiwamo vya Jamhuri Morogoro na Dodoma, Sokoine Mbeya, Alli Hassan Mwinyi Tabora, Kirumba Mwanza na kwingineko.
Unaposikia uwanja umefungiwa zaidi ya mara mbili unaanza kujiuliza tatizo nini ambalo haliishi na nani hasa mmiliki wa uwanja huo au viwanja hivyo, jibu unalipata kwamba kuna taaisi moja kubwa inaitwa CCM ambayo inajipambanua kwa sera za maendeleo ya michezo.
Ni vyema sasa taasisi hii ijitathmini na ianze kuweka nguvu katika maboresho ya viwanja vyake ili kuendana na sera yake ya maendeleo ya michezo.
Tofauti na hivyo sera hiyo inakuwa haina maana au haitekelezeki kama eneo muhimu katika maendeleo ya michezo yaani uwanja haupewi thamani yake.
Kimataifa Viwanja kufungiwa, wamiliki wajitathmini
Viwanja kufungiwa, wamiliki wajitathmini
Related posts
Read also
