Na Hassan Kingu
Mjadala umekuwa ukiibuka na kuzama kuhusu mabeki wa Simba na timu ya taifa ya Tanzania, Shomari Kapombe anayecheza kulia na Mohamed Hussein ‘Zimbwe Junior’ anayecheza kushoto.
Mjadala huu huibuka makosa yanapotokea halafu mmoja kati ya wachezaji hao akahusika, si tu mchezaji huyo atalaumiwa kwa makosa ya kiufundi yaliyotokea bali hoja kwamba amechoka au umri umeenda itaibuka.
Watacheza vizuri wataisaidia timu, watasifiwa lakini mmoja wao akifanya kosa iwe kazidiwa ujanja na mchezaji wa timu pinzani au hata kacheza rafu, ataambiwa umri umeenda au ameanza kuchoka au ameshajichokea.
Ni bahati mbaya sana wachezaji hawa hawasifiwi kwa namna walivyodumu katika namba zao kwa muda mrefu jambo ambalo limekuwa likiwashinda wachezaji wengi hasa wa kitanzania.
Uwezo ambao wamekuwa wakiuonesha ni jambo la kusifiwa, wamekuwa wakitoa ushawishi kwa makocha kadhaa wa Simba ambao wameweza kuwaamini licha ya lawama za msimu wanazotupiwa.
Mfano ni hivi karibuni Kapombe alipokosa bao katika mechi ya fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya RS Berkane, bao ambalo pengine lingeweza kuwafanya Simba wapate nguvu zaidi ya kuifikisha mechi katika hatua ya penalti tano tano.
Kapombe alikosa bao hilo akiwa karibu kabisa na kipa baada ya kuruka na kuupiga mpira kichwa lakini kwa mshangao wa wengi mpira ulikwenda nje ya lango.
Jibu la haraka haraka walilokuwa nalo baadhi ya mashabiki wa Simba ni kwamba mchezaji huyo amechoka, umri umeenda, mikimbio yake ya kupanda kutafuta ushindi na kurudi kujihami vyote vilionekana bure.
Juhudi zake licha ya kuwa ni beki lakini akafika karibu na kipa na kuwa sababu ya shambulizi hilo vyote hivyo havikuonekana, mashabiki hawakutaka kuamini kwamba hilo ni kosa la kawaida kwa mchezaji yeyote badala yake sababu iliyokuwa rahisi ni kwamba amechoka.
Kelele hizo za baadhi ya mashabiki kuhusu Kapombe na Zimbwe Jr ni za muda mrefu lakini makocha wote waliopita Simba wameendelea kuwaamini na kuwapa nafasi katika kikosi cha kwanza.
Msimamo huo wa makocha tofauti waliopita Simba miaka ya karibuni utoshe kuwafanya mashabiki wajiulize mara mbili mbili kuhusu wachezaji hao wawili, je ni kweli wamechoka kama tunavyoaminishana vijiweni?
Na kama kweli wamechoka kwa nini makocha wanawaamini na kama tumejiaminisha wamechoka badala ya kuwalaumu wakati huu wakiaminiwa na makocha tena makocha wa kigeni, ni vyema tukafikiria wachezaji mbadala wa ndani au nje tunaoamini wanaweza kuchukua nafasi zao.
Hadithi ya Kapombe, Zimbwe wamechoka ni ya muda mrefu lakini wachezaji hao wameendelea kuaminiwa na makocha kuanzia Juma Mgunda na wengine waliopita hadi, Robertinho, Abdelhak Benchikha na sasa Fadlu Davids.
Kuaminiwa kwa wachezaji hao na makocha kutoshe kutukumbusha kwamba bado wana vitu na ndio maana Simba imeweka rekodi ya kufikia hatua ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika mara tatu na juzi juzi tu imefikia hatua ya fainali Kombe la Shirikisho Afrika ikiwa ni mara ya kwanza tangu ifikie hatua hiyo katika mashindano ya hadhi hiyo mwaka 1993.
Ifahamike kwamba si wachezaji wote wenye uwezo wa kudumu katika namba zao kwa muda mrefu na kuaminiwa na makocha kwa miaka 10 au zaidi.
Mwaka 1987, Yanga ilimsajili beki wa kushoto Ken Mkapa, wamedumu naye kwa miaka 11, akiwa katika ubora kwenye nafasi yake hadi kuwa nahodha na baadaye kustaafu mwaka 1998 baada ya kuwa tegemeo Yanga na timu ya taifa ya Tanzania.
Real Madrid walikuwa na beki wa kushoto, Roberto Carlos, aliitawala nafasi hiyo kwa miaka 10 hadi 11 na hadi anaondoka mwaka 2007 aliondoka kwa heshima, hadhi yake ikiwa juu huku baadhi ya mashabiki wakipata tabu kuamini kama timu yao inaweza kuwa na beki wa hadhi yake atakayeimudu vyema nafasi hiyo.
Baada ya Carlos aliibuka Marcelo huyu naye aliitawala nafasi ya beki wa kushoto Real Madrid akicheza kwa mafanikio kwa miaka 14 hadi 15, kuanzia 2007 na hadi anaondoka 2022 aliondoka kwa heshima akiweka rekodi ya kuwa beki aliyedumu na kuitawala nafasi yake kwa kipindi kirefu.
Carlos na Marcelo ambao wote ni Wabrazili pia walitamba katika timu yao ya taifa na wameondoka wakiwa mashujaa na kupongezwa kama ilivyokuwa kwa Ken Mkapa akiwa Yanga.
Kwa hiyo tuwapongeze kina Kapombe na Zimbwe kwa kudumu katika nafasi zao kwa muda mrefu, Kapombe bila shaka anaisogelea miaka 10 Simba akiwa bora katika nafasi yake wakati Zimbwe tayari ameifikia miaka hiyo akiwa bora na mwenye mafanikio makubwa.