Paris, Ufaransa
Watu wawili wamefariki dunia huku mamia wakishikiliwa na polisi nchini Ufaransa baada ya mashabiki wa klabu ya Paris Saint-Germain (PSG) kusherehekea ushindi wa taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya.
PSG walifanikiwa kubeba taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya usiku wa Jumamosi Mei 31, 2025 baada ya kuichapa Inter Milan ya Italia mabao 5-0.
Taarifa ya polisi ilieleza kuwa kijana mmoja wa miaka 17 katika mji wa Dax alifariki Jumamosi usiku kwa kuchomwa na kitu kifuani wakati mashabiki wa PSG wakiwa katika shmrashamra za ushindi huo.
Mtu mwingine aliyeuawa ni kijana wa miaka 23 ambaye alikuwa akiendesha baiskeli ndogo katikati ya jiji la Paris ambaye kifo chake kilitokea baada ya kugongwa na gari.
Mashabiki wa PSG walionekana kuwehuka na ushindi huo wa kihistoria na baadhi yao kufikia hatua ya kuvunja vituo vya mabasi na kuchoma moto magari.
Klabu ya PSG ilitoa taarifa kulaani matukio hayo ya vurugu na kuongeza kuwa yanakwenda kinyume na maadili ya klabu hiyo na kwa namna yoyote ni vitendo ambavyo haviwakilishi sehemu kubwa ya mashabiki wao.
Kwa upande wake Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron alisema vurugu hizo hazikubaliki na hazina uhalali wowote na wote waliohusika wataadhibiwa.
Mashabiki wa PSG hata hivyo waliendelea na maandamano yao ya kusherehekea ushindi hadi siku iliyofuata yaani Jumapili ingawa idadi ya maofisa usalama iliongezeka katika mitaa waliyokuwa mashabiki hao.
Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Ndani ilieleza kuwa polisi 20 na maofisa saba ya kikosi cha zimamoto walijeruhiwa huku jumla ya magari 264 yakichomwa moto katika matukio yaliyotokea mapema Jumapili.
Kimataifa Ushindi wa PSG, wawili wauawa, magari yachomwa moto
Ushindi wa PSG, wawili wauawa, magari yachomwa moto
Read also
