Na mwandishi wetu
Kocha Mkuu wa Timu ya Taifa ya Wavulana chini ya miaka 18, Habibu Kondo (pichani), amesema kuwa ushindi wa bao 1-0 walioupata dhidi ya Uganda haukuwa rahisi.
Kondo alisema kwamba katika ushindi huo alifurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na vijana wake hao kwenye michuani ya Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) inayoendelea nchini Kenya.
Ushindi huo wa jana umeifanya Tanzania kupanda kileleni mwa Kundi B kwa pointi tatu sawa na Zanzibar ambao pia waliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Sudan Kusini.
“Tunashukuru tumepata ushindi kwenye mchezo wa leo (jana) maana ilikuwa mechi ngumu sana tulijua hilo tangu tulipokuwa tunatoka nyumbani.
“Tulikuwa na mipango yetu ya ushindi dhidi ya Uganda na ndicho kilichokuwa, tulianza vizuri lakini baadae mechi ilikuja kubadilika sababu ya mvua ilikuja kuharibu mchezo, yote kwa yote tunamshukuru Mungu kupata matokeo kwa mchezo wa kwanza,” alisema Kondo.
Alisema unapoanza kwa matokeo mazuri inajenga hali ya kujiamini kwa timu kwamba mechi nyingine inayofuata mtaichezaje.
“Sisi tulijitayarisha kuutawala mchezo kwa kutengeneza nafasi kuanzia nyuma ndicho tulichokifanya kipindi cha kwanza lakini kipindi cha pili kazi ilikuwa kupora mipira na kupiga kwenye lango la wapinzani na kwenda kusapoti shambulizi,” alisema Kondo.
