Na mwandishi wetu
Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Maxi Nzengeli (pichani) ameishukuru klabu hiyo kutokana na mafanikio ya mapema aliyoanza kuyapata kwa kuibuka Mchezaji Bora wa Ligi Kuu NBC mwezi Agosti.
Nzengeli aliibuka kidedea katika kinyang’anyiro hicho dhidi ya Stephane Aziz Ki wa Yanga na Jean Baleke wa Simba.
Mchezaji huyo alifunga mabao mawili na kutoa pasi moja ya bao katika mechi mbili dhidi ya KMC na JKT Tanzania ilizocheza Yanga katika mwezi huo na kila mechi waliibuka na ushindi wa mabao 5-0.
Nzengeli raia wa DR Congo aliyetua Yanga msimu huu alisema anawashukuru wote waliohusika kupata mafanikio hayo kuanzia wachezaji wenzake, mashabiki na zaidi benchi la ufundi chini ya kocha Miguel Gamondi ambaye naye aliibuka kocha bora wa mwezi huo.
“Nashukuru Mungu kwa kupata tuzo ya mchezaji bora wa mwezi, lakini pia nawashukuru sana benchi la ufundi, nasema asante kwa wachezaji wenzangu wa Yanga, viongozi wa klabu na pia mashabiki wa timu kwa hiki nilichokipata,” alisema Maxi.
