Manchester, England
Beki Phil Jones ataondoka Man United mkataba wake utakapoisha majira ya kiangazi msimu huu akiwa amepitia kipindi kigumu miaka ya karibuni cha kuandamwa na majanga ya kuwa majeruhi.
“Nimepambana kwa bidii bila kuchoka, katika hali ya kawaida sina nilichokiacha, nilijaribu kurudi katika ubora haraka kadri nilivyoweza, katika miaka yangu ya mwisho nimekuwa nikikosekana kila mara,” alisema Jones katika barua yake kwa mashabiki wa klabu hiyo.
Jones ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 31, alijiunga na Man United mwaka 2011 akitokea Blackburn Rovers na alikuwamo katika kikosi kilichobeba taji la Ligi Kuu England (EPL) msimu wa 2012-13.
Beki huyo ana rekodi ya kuichezea Man United mara 229 na kufunga mabao sita hapo hapo akiichezea timu ya Taifa ya England mechi 27.
Mara ya mwisho kuonekana akicheza ilikuwa msimu uliopita katika mechi dhidi ya Brentford ambayo Man United ilitoka na ushindi wa mabao 3-0 lakini tangu hapo amekuwa nje kutokana na kuwa majeruhi.
“Natamani ningecheza zaidi, natamani ningejitoa katika kikosi hiki kikubwa nilichokuwa miongoni mwa wachezaji, ninasema kutoka ndani ya moyo wangu kwamba nimefanya kila nilichoweza,” alisema Jones.
“Nimekuwa na wakati mgumu miaka michache ya karibuni, hilo sina sababu ya kulificha,” aliongeza na kusisitiza kwamba anajiona kama ameiangusha timu na anaona vigumu hata kuzungumza na wachezaji wenzake kwa sababu ya maumivu ya kushindwa kuwasaidia.
Kimataifa Phil Jones aaga mashabiki Man United
Phil Jones aaga mashabiki Man United
Read also
